29
Kufanya Upya Agano
Haya ndiyo maneno ya Agano Bwana aliyomwagiza Mose kufanya na Waisraeli huko Moabu, kuwa nyongeza ya Agano alilofanya nao huko Horebu.
Mose akawaita Waisraeli wote akawaambia:
 
Macho yenu yameona yale yote Bwana aliyofanya kwa Mfalme Farao huko Misri, kwa maafisa wake wote na kwa nchi yake yote. Kwa macho yenu wenyewe mliona yale majaribu makubwa, ishara zile za miujiza na maajabu makubwa. Lakini mpaka leo Bwana hajawapa akili ya kuelewa au macho yanayoona au masikio yanayosikia. Kwa muda wa miaka arobaini niliyowaongoza jangwani, nguo zenu hazikuchakaa, wala viatu miguuni mwenu. Hamkula mkate na hamkunywa divai wala kileo chochote. Nilifanya hivi ili mpate kujua kuwa mimi ndimi Bwana Mungu wenu.
Wakati mlipofika mahali hapa, Sihoni mfalme wa Heshboni na Ogu mfalme wa Bashani walikuja kupigana dhidi yetu, lakini tuliwashinda. Tuliichukua nchi yao na kuwapa Wareubeni, Wagadi na nusu ya kabila la Manase kama urithi wao.
Fuateni kwa bidii masharti ya Agano hili, ili kwamba mweze kustawi katika kila kitu mnachofanya. 10 Ninyi nyote leo mnasimama mbele za Bwana Mungu wenu; mkiwa viongozi na wakuu wenu, wazee na maafisa wenu, na wanaume wengine wote wa Israeli, 11 pamoja na watoto wenu, wake zenu na pia wageni waishio katika kambi zenu wanaowapasulia kuni na kuwachotea maji. 12 Mnasimama hapa ili kufanya Agano na Bwana Mungu wenu, Agano ambalo Mungu analifanya nanyi siku hii ya leo na kulitia muhuri kwa kiapo, 13 kuwathibitisha ninyi siku hii ya leo kama taifa lake, ili aweze kuwa Mungu wenu kama alivyowaahidi na kama alivyowaapia baba zenu Abrahamu, Isaki na Yakobo. 14 Ninafanya Agano hili pamoja na kiapo chake, sio na ninyi tu 15 mnaosimama hapa na sisi leo mbele za Bwana Mungu wetu, bali pia pamoja na wale ambao hawapo hapa leo.
16 Ninyi wenyewe mnajua jinsi tulivyoishi nchini Misri na jinsi tulivyopita katikati ya nchi mpaka tukafika hapa. 17 Mliona miongoni mwao vinyago vyao vya kuchukiza na sanamu za miti na mawe, za fedha na dhahabu. 18 Hakikisheni kwamba hakuna mwanaume au mwanamke, ukoo au kabila miongoni mwenu leo ambalo moyo wake utamwacha Bwana Mungu wetu, kwenda kuabudu miungu ya mataifa hayo. Hakikisheni hakuna mzizi miongoni mwenu unaotoa sumu chungu ya namna hii.
19 Wakati mtu wa namna hii asikiapo maneno ya kiapo hiki, hujibariki mwenyewe na kisha hufikiri, “Nitakuwa salama, hata kama nikiendelea kuifuata njia yangu mwenyewe.” Hili litaleta maafa juu ya nchi iliyonyeshewa sawasawa na nchi kame. 20  Bwana kamwe hatakuwa radhi kumsamehe, ghadhabu na wivu wa Mungu vitawaka dhidi ya mtu huyo. Laana zote zilizoandikwa katika kitabu hiki zitamwangukia na Bwana atafuta jina lake chini ya mbingu. 21  Bwana atamtwaa peke yake kutoka makabila ya Israeli kwa maangamizo, kulingana na laana zote za Agano zilizoandikwa kwenye Kitabu hiki cha Sheria.
22 Watoto wako watakaofuata baada yako katika vizazi vya baadaye na wageni ambao watakuja kutoka nchi za mbali, wataona maafa, yaliyoipata nchi na magonjwa ambayo Bwana aliyaleta juu yake. 23 Nchi yote itakuwa jaa linaloungua la chumvi na kiberiti: hakutakuwa kilichopandwa, hakutakuwa kinachochipua, wala hakutakuwa mimea inayoota juu yake. Itakuwa kama maangamizo ya Sodoma na Gomora, Adma na Seboimu, ambazo Bwana aliangamiza kwa hasira kali. 24 Mataifa yote yatauliza: “Kwa nini Bwana amefanya hivi juu ya nchi hii? Kwa nini hasira hii kali ikawaka?”
25 Na jibu litakuwa: “Ni kwa sababu watu hawa waliacha Agano la Bwana, Mungu wa baba zao, Agano alilofanya nao wakati alipowatoa katika nchi ya Misri. 26 Walienda zao na kuabudu miungu mingine na kuisujudia, miungu wasioijua, miungu ambayo Mungu hakuwapa. 27 Kwa hiyo hasira ya Bwana ikawaka dhidi ya nchi hii, hivyo Mungu akaleta juu yake laana zote zilizoandikwa katika kitabu hiki. 28 Katika hasira kali na katika ghadhabu kuu Bwana aliwangʼoa kutoka nchi yao na kuwasukumia katika nchi nyingine, kama ilivyo sasa.”
29 Mambo ya siri ni ya Bwana Mungu wetu, bali yaliyofunuliwa ni yetu na watoto wetu milele, ili tuweze kuyafanya maneno yote ya sheria hii.