35
Furaha Ya Waliokombolewa 
 
1 Jangwa na nchi kame vitafurahi;  
nyika itashangilia na kuchanua maua.  
Kama waridi,  
2 litachanua maua,  
litashangilia sana na kupaza sauti kwa furaha.  
Litapewa utukufu wa Lebanoni,  
fahari ya Karmeli na Sharoni;  
wataona utukufu wa Bwana,  
fahari ya Mungu wetu.   
   
 
3 Itieni nguvu mikono iliyo dhaifu,  
yafanyeni imara magoti yaliyolegea,   
4 waambieni wale wenye mioyo ya hofu,  
“Kuweni hodari, msiogope;  
tazama, Mungu wenu atakuja,  
pamoja na malipo ya Mungu,  
atakuja na kuwaokoa ninyi.”   
   
 
5 Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa  
na masikio ya viziwi yatazibuliwa.   
6 Ndipo kilema atarukaruka kama kulungu,  
nao ulimi wa aliye bubu utapaza sauti kwa shangwe.  
Maji yatatiririka kwa kasi katika nyika,  
na vijito katika jangwa.   
7 Mchanga wa moto utakuwa bwawa la maji,  
ardhi yenye kiu itabubujika chemchemi.  
Maskani ya mbweha walikolala hapo awali  
patamea majani, matete na mafunjo.   
   
 
8 Nako kutakuwa na njia kuu,  
nayo itaitwa Njia ya Utakatifu.  
Wasio safi hawatapita juu yake;  
itakuwa ya wale watembeao katika Njia ile;  
yeye asafiriye juu yake,  
ajapokuwa mjinga, hatapotea.   
9 Huko hakutakuwepo na simba,  
wala mnyama mkali hatapita njia hiyo,  
wala hawatapatikana humo.  
Ila waliokombolewa tu ndio watakaopita huko,   
10 waliokombolewa na Bwana watarudi.  
Wataingia Sayuni wakiimba;  
furaha ya milele itakuwa juu ya vichwa vyao.  
Watapata furaha na shangwe;  
huzuni na majonzi vitakimbia.