54
Utukufu Wa Baadaye Wa Sayuni
“Imba, ewe mwanamke tasa,
wewe ambaye kamwe hukuzaa mtoto;
paza sauti kwa kuimba, piga kelele kwa furaha,
wewe ambaye kamwe hukupata utungu;
kwa sababu watoto wa mwanamke aliyeachwa ukiwa ni wengi
kuliko wa mwanamke mwenye mume,”
asema Bwana.
“Panua mahali pa hema lako,
tandaza mapazia ya hema lako uyaeneze mbali,
wala usiyazuie;
ongeza urefu wa kamba zako,
imarisha vigingi vyako.
Kwa maana utaenea upande wa kuume
na upande wa kushoto;
wazao wako watayamiliki mataifa
na kukaa katika miji yao iliyoachwa ukiwa.
 
“Usiogope, wewe hutaaibika.
Usiogope aibu, wewe hutaaibishwa.
Wewe utasahau aibu ya ujana wako,
wala hutakumbuka tena mashutumu ya ujane wako.
Kwa maana Muumba wako ndiye mume wako,
Bwana Mwenye Nguvu Zote ndilo jina lake,
yeye Aliye Mtakatifu wa Israeli ni Mkombozi wako,
yeye anaitwa Mungu wa dunia yote.
Bwana atakuita urudi
kana kwamba ulikuwa mke aliyeachwa na kuhuzunishwa rohoni;
kama mke aliyeolewa bado angali kijana
na kukataliwa,” asema Mungu wako.
“Kwa kitambo kidogo nilikuacha,
lakini kwa huruma nyingi nitakurudisha.
Katika ukali wa hasira
nilikuficha uso wangu kwa kitambo,
lakini kwa fadhili za milele
nitakuwa na huruma juu yako,”
asema Bwana Mkombozi wako.
 
“Kwangu mimi jambo hili ni kama siku za Noa,
nilipoapa kuwa maji ya Noa kamwe hayatafunika tena dunia.
Hivyo sasa nimeapa sitawakasirikia ninyi,
kamwe sitawakemea tena.
10 Ijapotikisika milima, na vilima viondolewe,
hata hivyo upendo wangu usiokoma kwenu hautatikisika,
wala agano langu la amani halitaondolewa,”
asema Bwana, mwenye huruma juu yenu.
 
11 “Ewe mji uliyeteswa, uliyepigwa kwa dhoruba na usiyetulizwa,
nitakujenga kwa almasi, nitaweka misingi yako kwa yakuti samawi.
12 Nitafanya minara yako ya akiki,
malango yako kwa vito vingʼaavyo,
nazo kuta zako zote za vito vya thamani.
13 Watoto wako wote watafundishwa na Bwana,
nayo amani ya watoto wako itakuwa kuu.
14 Kwa haki utathibitika:
Kuonewa kutakuwa mbali nawe;
hutaogopa chochote.
Hofu itakuwa mbali nawe;
haitakukaribia wewe.
15 Kama mtu yeyote akikushambulia,
haitakuwa kwa ruhusa yangu;
yeyote akushambuliaye
atajisalimisha kwako.
 
16 “Tazama, ni mimi niliyemuumba mhunzi,
yeye afukutaye makaa kuwa moto,
na kutengeneza silaha inayofaa kwa kazi yake.
Tena ni mimi niliyemwambia mharabu
kufanya uharibifu mwingi.
17 Hakuna silaha itakayofanyizwa dhidi yako
itakayofanikiwa,
nawe utauthibitisha kuwa mwongo
kila ulimi utakaokushtaki.
Huu ndio urithi wa watumishi wa Bwana
na hii ndiyo haki yao itokayo kwangu,”
asema Bwana.