17
Sanamu Za Mika
Palikuwa na mtu aliyeitwa Mika ambaye aliishi katika vilima vya Efraimu. Akamwambia mama yake, “Zile shekeli 1,100* za fedha zilizochukuliwa kwako, ambazo nilisikia ukizinenea maneno ya laana, hizi hapa; mimi ndiye niliyezichukua, lakini sasa ninakurudishia.”
Ndipo mama yake akamwambia, “Bwana na akubariki, mwanangu.”
Alipozirudisha zile shekeli 1,100 za fedha kwa mama yake, mama yake akamwambia, “Mimi nimeiweka fedha hii wakfu kwa Bwana kwa ajili ya mwanangu kutengenezea kinyago cha kuchonga na sanamu ya kusubu. Mimi nitakurudishia wewe.”
Hivyo akamrudishia mama yake ile fedha, naye mama yake akachukua shekeli mia mbili za hiyo fedha na kumpa mfua fedha, ambaye aliifanyiza kinyago na sanamu. Navyo vikawekwa ndani ya nyumba ya Mika.
Basi Mika alikuwa na mahali pa kuabudia miungu, akatengeneza naivera, pamoja na vinyago, na kumweka mmoja wa wanawe kuwa kuhani wake. Katika siku hizo Israeli hawakuwa na mfalme, kila mmoja akafanya kama alivyoona vyema machoni pake mwenyewe.
Basi palikuwa na kijana mmoja wa Bethlehemu ya Yuda. Yeye alikuwa Mlawi aliyeishi miongoni mwa kabila la Yuda. Huyu kijana akatoka katika mji huo wa Bethlehemu ya Yuda na kutafuta mahali pengine ambapo angeweza kuishi. Alipokuwa akisafiri, akafika nyumbani kwa Mika katika vilima vya Efraimu.
Mika akamuuliza, “Wewe umetoka wapi?”
Akamjibu, “Mimi ni Mlawi kutoka Bethlehemu ya Yuda, ninatafuta mahali pa kuishi.”
10 Ndipo Mika akamwambia, “Ishi pamoja nami, uwe baba yangu na kuhani wangu, nami nitakupa shekeli kumi za fedha, nguo na chakula.” 11 Hivyo yule Mlawi akakubali kuishi pamoja naye, naye huyo kijana akawa kwake kama mmoja wa wanawe. 12 Hivyo Mika akamweka wakfu huyo kijana Mlawi, naye huyo akawa kuhani wake na kuishi nyumbani mwake. 13 Ndipo Mika akasema, “Sasa najua Bwana atanitendea mema, kwa kuwa Mlawi huyu amekuwa kuhani wangu.”
* 17:2 Shekeli 1,100 za fedha ni sawa na kilo 13 za fedha. 17:4 Shekeli 200 za fedha ni sawa na kilo 2.3 za fedha. 17:10 Shekeli 10 za fedha ni sawa na gramu 115 za fedha.