22
Hukumu Dhidi Ya Wafalme Waovu
Hili ndilo asemalo Bwana: “Shuka kwenye jumba la kifalme la mfalme wa Yuda, utangaze ujumbe huu huko: ‘Sikia neno la Bwana, ee mfalme wa Yuda, wewe uketiye kwenye kiti cha enzi cha Daudi: wewe, maafisa wako na watu wako mnaopitia malango haya. Hili ndilo Bwana asemalo: Tenda haki na adili. Mwokoe mkononi mwa mdhalimu yeye aliyetekwa nyara. Usimtendee mabaya wala ukatili mgeni, yatima au mjane, wala usimwage damu isiyo na hatia mahali hapa. Kwa kuwa ukiwa mwangalifu kushika maagizo haya, ndipo wafalme watakaokalia kiti cha enzi cha Daudi watakapoingia kupitia malango ya jumba hili la kifalme, wakiwa wamepanda magari na farasi, huku wakifuatana na maafisa wao na watu wao. Lakini kama hutayatii maagizo haya, asema Bwana, ninaapa kwa nafsi yangu kwamba jumba hili litakuwa gofu.’ ”
Kwa kuwa hili ndilo Bwana asemalo kuhusu jumba la kifalme la mfalme wa Yuda:
“Ingawa uko kama Gileadi kwangu,
kama kilele cha Lebanoni,
hakika nitakufanya uwe kama jangwa,
kama miji ambayo haijakaliwa na watu.
Nitawatuma waharabu dhidi yako,
kila mtu akiwa na silaha zake,
nao watazikata boriti zako nzuri za mierezi
na kuzitupa motoni.
“Watu kutoka mataifa mengi watapitia karibu na mji huu na kuulizana, ‘Kwa nini Bwana amefanya jambo la namna hii juu ya mji huu mkubwa?’ Nalo jibu litakuwa: ‘Kwa sababu wameliacha agano la Bwana, Mungu wao, na wameabudu na kuitumikia miungu mingine.’ ”
10 Usimlilie yeye aliyekufa, wala usimwombolezee;
badala yake, afadhali umlilie kwa uchungu
yule aliyepelekwa uhamishoni,
kwa sababu kamwe hatairudia
wala kuiona tena nchi yake alikozaliwa.
11 Kwa kuwa hili ndilo asemalo Bwana kuhusu Shalumu* mwana wa Yosia, aliyeingia mahali pa baba yake kuwa mfalme wa Yuda, lakini ameondoka mahali hapa: “Yeye kamwe hatarudi tena. 12 Atafia huko mahali walipompeleka kuwa mateka; hataiona tena nchi hii.”
13 “Ole wake yeye ajengaye jumba lake la kifalme kwa njia ya dhuluma,
vyumba vyake vya juu kwa udhalimu,
akiwatumikisha watu wa nchi yake pasipo malipo,
bila kuwalipa kwa utumishi wao.
14 Asema, ‘Nitajijengea jumba kuu la kifalme,
na vyumba vya juu vyenye nafasi kubwa.’
Hivyo anaweka ndani yake madirisha makubwa,
huweka kuta za mbao za mierezi,
na kuipamba kwa rangi nyekundu.
 
15 “Je, inakufanya kuwa mfalme
huko kuongeza idadi ya mierezi?
Je, baba yako hakuwa na chakula na kinywaji?
Alifanya yaliyo sawa na haki,
hivyo yeye akafanikiwa katika yote.
16 Aliwatetea maskini na wahitaji,
hivyo yeye akafanikiwa katika yote.
Je, hiyo si ndiyo maana ya kunijua mimi?”
asema Bwana.
17 “Lakini macho yako na moyo wako vimeelekezwa tu
katika mapato ya udhalimu,
kwa kumwaga damu isiyo na hatia,
kwa uonevu na ukatili.”
18 Kwa hiyo hili ndilo asemalo Bwana kuhusu Yehoyakimu mwana wa Yosia mfalme wa Yuda:
“Hawatamwombolezea wakisema:
‘Ole, ndugu yangu! Ole, umbu langu!’
Hawatamwombolezea wakisema:
‘Ole, bwana wangu! Ole, fahari yake!’
19 Atazikwa maziko ya punda:
ataburutwa na kutupwa
nje ya malango ya Yerusalemu.”
 
20 “Panda Lebanoni ukapige kelele,
sauti yako na isikike huko Bashani,
piga kelele toka Abarimu,
kwa kuwa wote waliojiunga nawe wameangamizwa.
21 Nilikuonya wakati ulipojisikia kwamba uko salama,
lakini ulisema, ‘Mimi sitasikiliza!’
Hii imekuwa kawaida yako tangu ujana wako;
hujanitii mimi.
22 Upepo utawaondoa wachungaji wako wote,
na wale ulioungana nao wataenda uhamishoni.
Kisha utaaibika na kufedheheka
kwa sababu ya uovu wako wote.
23 Wewe uishiye Lebanoni,
wewe uliyetulia kwenye majengo ya mierezi,
tazama jinsi utakavyoomboleza
maumivu makali yatakapokupata,
maumivu kama yale ya mwanamke
mwenye utungu wa kuzaa!
24 “Hakika kama niishivyo,” asema Bwana, “hata kama wewe, Yekonia mwana wa Yehoyakimu mfalme wa Yuda, ungekuwa pete yangu ya muhuri katika mkono wangu wa kuume, bado ningekungʼoa hapo. 25 Nitakutia mikononi mwa wale wanaotafuta uhai wako, wale unaowaogopa, yaani Nebukadneza mfalme wa Babeli na kwa Wakaldayo. 26 Nitakutupa mbali wewe na mama aliyekuzaa mwende katika nchi nyingine, ambayo hakuna hata mmoja wenu aliyezaliwa huko, nanyi mtafia huko. 27 Kamwe hamtarudi katika nchi mliyotamani kuirudia.”
28 Je, huyu mtu Yekonia ni chungu kilichodharauliwa,
chungu kilichovunjika,
chombo kisichotakiwa na mtu yeyote?
Kwa nini yeye na watoto wake watupwe nje kwa nguvu,
na kutupwa kwenye nchi wasioijua?
29 Ee nchi, nchi, nchi,
sikia neno la Bwana!
30 Hili ndilo Bwana asemalo:
“Mwandike huyu mtu kama asiye na mtoto,
mtu ambaye hatafanikiwa maisha yake yote,
kwa maana hakuna mtoto wake atakayefanikiwa,
wala kukaa kwenye kiti cha enzi cha Daudi
wala kuendelea kutawala katika Yuda.”
* 22:11 Shalumu ndiye pia anaitwa Yehoahazi. 22:24 Yekonia au Konia ni jina jingine la Yehoyakini.