3
Walawi
Hii ni hesabu ya jamaa ya Aroni na Mose kwa wakati ambao Bwana alizungumza na Mose katika Mlima Sinai.
 
Majina ya wana wa Aroni yalikuwa: Nadabu mzaliwa wa kwanza na Abihu, Eleazari na Ithamari. Hayo yalikuwa majina ya wana wa Aroni, makuhani wapakwa mafuta, waliokuwa wamesimikwa kuhudumu kama makuhani. Hata hivyo Nadabu na Abihu walikufa mbele za Bwana walipotoa sadaka kwa moto usioruhusiwa mbele zake katika Jangwa la Sinai. Hawakuwa na wana; kwa hiyo Eleazari na Ithamari walihudumu peke yao kama makuhani wakati wote wa maisha ya Aroni baba yao.
Bwana akamwambia Mose, “Walete watu wa kabila la Lawi mbele ya Aroni kuhani ili wamsaidie. Watafanya huduma kwa ajili yake na kwa jumuiya yote katika Hema la Kukutania kwa kufanya kazi za Maskani. Watatunza samani zote za Hema la Kukutania, wakitimiza wajibu wa kuhudumia Waisraeli kwa kufanya kazi ya Maskani. Wakabidhi Walawi kwa Aroni na wanawe; hao ndio Waisraeli ambao wanakabidhiwa kwake kabisa. 10 Waweke Aroni na wanawe kuhudumu kama makuhani; mtu mwingine yeyote atakayesogea mahali patakatifu ni lazima auawe.”
11  Bwana akamwambia Mose, 12 “Nimewatwaa Walawi kutoka miongoni mwa Waisraeli badala ya mzaliwa wa kwanza wa kiume wa kila mwanamke wa Mwisraeli. Walawi ni wangu, 13 kwa kuwa wazaliwa wote wa kwanza ni wangu. Nilipowaua wazaliwa wa kwanza huko Misri, nilimtenga kila mzaliwa wa kwanza katika Israeli awe wangu, akiwa mwanadamu au mnyama. Watakuwa wangu. Mimi ndimi Bwana.”
14  Bwana akamwambia Mose katika Jangwa la Sinai, 15 “Wahesabu Walawi kwa jamaa zao na koo zao. Mhesabu kila mwanaume mwenye umri wa mwezi mmoja au zaidi.” 16 Kwa hiyo Mose akawahesabu, kama alivyoamriwa na neno la Bwana.
17 Haya yalikuwa majina ya wana wa Lawi:
Gershoni, Kohathi na Merari.
18 Haya ndiyo yaliyokuwa majina ya koo za Wagershoni:
Libni na Shimei.
19 Koo za Wakohathi zilikuwa ni:
Amramu, Ishari, Hebroni na Uzieli.
20 Koo za Wamerari zilikuwa ni:
Mahli na Mushi.
Hizi ndizo zilizokuwa koo za Walawi, kufuatana na jamaa zao.
 
21 Kulikuwa na koo za Walibni na Washimei kwa Gershoni; hizi ndizo zilizokuwa koo za Wagershoni. 22 Idadi ya waume wote waliokuwa na mwezi mmoja au zaidi waliohesabiwa walikuwa 7,500. 23 Ukoo wa Wagershoni walitakiwa kuweka kambi zao upande wa magharibi, nyuma ya Maskani. 24 Kiongozi wa jamaa za Wagershoni alikuwa Eliasafu mwana wa Laeli. 25 Katika Hema la Kukutania, Wagershoni walikuwa na wajibu wa kutunza Maskani na hema, vifuniko vyake, pazia katika mlango wa kuingilia ndani ya Hema la Kukutania, 26 mapazia ya ua, pazia katika ingilio la ua unaozunguka Maskani na madhabahu, pamoja na kamba, na kila kinachohusika kwa matumizi yake.
 
27 Kwa Kohathi kulikuwepo koo za Waamramu, Waishari, Wahebroni na Wauzieli; hizi ndizo zilizokuwa koo za Wakohathi. 28 Hesabu ya waume wote wenye mwezi mmoja au zaidi ilikuwa watu 8,600. Wakohathi waliwajibika kutunza mahali patakatifu. 29 Koo za Wakohathi zilitakiwa kuweka kambi zao upande wa kusini wa Maskani. 30 Kiongozi wa jamaa za koo za Wakohathi alikuwa Elisafani mwana wa Uzieli. 31 Waliwajibika kutunza Sanduku la Agano, meza, kinara cha taa, madhabahu, na vile vyombo vya mahali patakatifu vinavyotumika kuhudumu, pazia, na kila kitu kinachohusika na matumizi yake. 32 Kiongozi mkuu wa Walawi alikuwa Eleazari mwana wa kuhani, Aroni. Aliwekwa juu ya wale waliowajibika kutunza mahali patakatifu.
 
33 Kwa Merari kulikuwa na koo za Wamahli na Wamushi; hizi zilikuwa koo za Merari. 34 Hesabu ya waume wote wenye umri wa mwaka mmoja au zaidi waliohesabiwa walikuwa 6,200. 35 Kiongozi wa jamaa za koo za Wamerari alikuwa Surieli mwana wa Abihaili; hawa walitakiwa kuweka kambi zao upande wa kaskazini mwa Maskani. 36 Wamerari waliwekwa kutunza miimo ya Maskani, mataruma yake, nguzo, vitako na vifaa vyake vyote na kila kitu kilichohusika na matumizi yake, 37 na pia nguzo za ua unaozunguka pamoja na vitako vyake, vigingi vya hema na kamba zake.
 
38 Mose, na Aroni na wanawe walitakiwa kuweka kambi zao mashariki mwa Maskani, kuelekea mawio ya jua, mbele ya Hema la Kukutania. Wao walihusika na utunzaji wa mahali patakatifu kwa niaba ya Waisraeli. Mtu mwingine yeyote aliyepasogelea mahali patakatifu angeuawa.
 
39 Jumla ya hesabu ya Walawi waliohesabiwa na Mose na Aroni kwa amri ya Bwana, kufuatana na koo, pamoja na kila mume mwenye umri wa mwezi mmoja au zaidi, walikuwa 22,000.
 
40  Bwana akamwambia Mose, “Wahesabu wazaliwa wa kwanza wa kiume wote wa Waisraeli wenye umri wa mwezi mmoja au zaidi na uorodheshe majina yao. 41 Nitwalie Walawi badala ya wazaliwa wa kwanza wa Waisraeli, nayo mifugo ya Walawi badala ya wazaliwa wa mifugo ya Waisraeli. Mimi ndimi Bwana.”
42 Hivyo Mose akawahesabu wazaliwa wa kwanza wote wa Waisraeli, kama Bwana alivyomwamuru. 43 Jumla ya hesabu ya wazaliwa wa kwanza waume wenye umri wa mwezi mmoja au zaidi, walioorodheshwa kwa majina, walikuwa 22,273.
44  Bwana akamwambia Mose, 45 “Watwae Walawi badala ya wazaliwa wa kwanza wote wa Israeli, nayo mifugo ya Walawi badala ya mifugo yao. Walawi watakuwa wangu. Mimi ndimi Bwana. 46 Ili kukomboa wazao wa kwanza 273 wa Waisraeli ambao wamezidi hesabu ya Walawi, 47 kusanya shekeli tano* kwa kila mmoja, kufuatana na shekeli ya mahali patakatifu, ambayo ina uzito wa gera ishirini. 48 Mpe Aroni na wanawe hizo fedha kwa ajili ya ukombozi wa idadi ya Waisraeli waliozidi.”
49 Kwa hiyo Mose akakusanya fedha za ukombozi kutoka kwa wale ambao hesabu yao ilizidi wale waliokombolewa na Walawi. 50 Kutokana na wazaliwa wa kwanza wa Waisraeli alikusanya fedha yenye uzito wa shekeli 1,365 kufuatana na shekeli ya mahali patakatifu. 51 Mose akampa Aroni na wanawe ile fedha ya ukombozi, kama alivyoamriwa na neno la Bwana.
* 3:47 Shekeli tano ni sawa na gramu 55. 3:47 Gera 20 ni sawa na gramu 11. 3:50 Shekeli 1,365 ni sawa na kilo 15.5.