*
Zaburi 10
Sala Kwa Ajili Ya Haki
Kwa nini, Ee Bwana, unasimama mbali?
Kwa nini unajificha wakati wa shida?
 
Katika kiburi chake, mwovu humtesa maskini,
waovu na wanaswe katika hila wanazozitunga.
Hujivunia tamaa za moyo wake;
humbariki mlafi na kumtukana Bwana.
Katika kiburi chake, mwovu hamtafuti Mungu,
katika mawazo yake yote
hakuna nafasi ya Mungu.
Njia zake daima hufanikiwa;
hujivuna na amri zako ziko mbali naye,
huwacheka kwa dharau adui zake wote.
Anajisemea mwenyewe, “Hakuna kitakachonitikisa,
daima nitakuwa na furaha,
kamwe sitakuwa na shida.”
Kinywa chake kimejaa laana, uongo na vitisho;
shida na ubaya viko chini ya ulimi wake.
Huvizia karibu na vijiji;
kutoka mafichoni huwanasa wasio na hatia,
akivizia wapitaji.
Huvizia kama simba aliye mawindoni;
huvizia kumkamata mnyonge,
huwakamata wanyonge na kuwaburuza
katika wavu wake.
10 Mateka wake hupondwa, huzimia;
wanaanguka katika nguvu zake.
11 Anajisemea mwenyewe, “Mungu amesahau,
huficha uso wake na haoni kabisa.”
 
12 Inuka Bwana! Inua mkono wako, Ee Mungu.
Usiwasahau wanyonge.
13 Kwa nini mtu mwovu anamtukana Mungu?
Kwa nini anajiambia mwenyewe,
“Hataniita nitoe hesabu?”
14 Lakini wewe, Ee Mungu, unaona shida na huzuni,
umekubali kuyapokea mkononi mwako.
Mhanga anajisalimisha kwako,
wewe ni msaada wa yatima.
15 Vunja mkono wa mtu mwovu na mbaya,
mwite atoe hesabu ya maovu yake
ambayo yasingejulikana.
 
16  Bwana ni Mfalme milele na milele,
mataifa wataangamia watoke nchini mwake.
17 Unasikia, Ee Bwana, shauku ya wanaoonewa,
wewe huwatia moyo, na kusikiliza kilio chao,
18 ukiwatetea yatima na walioonewa,
ili mwanadamu, ambaye ni udongo, asiogopeshe tena.
* Zaburi 10: Zaburi hii ikiunganishwa na ya 9 zimetungwa kila beti likianzia na herufi ya alfabeti ya Kiebrania zikifuatana tangu Aleph (A) hadi Taw (T); zote ni 22.