Zaburi 17
Sala Ya Mtu Asiye Na Hatia
Sala ya Daudi.
Sikia, Ee Bwana, kusihi kwangu kwa haki,
sikiliza kilio changu.
Tega sikio kwa ombi langu,
halitoki kwenye midomo ya udanganyifu.
Hukumu yangu na itoke kwako,
macho yako na yaone yale yaliyo haki.
 
Ingawa unauchunguza moyo wangu na kunikagua usiku,
ingawa umenijaribu, hutaona chochote.
Nimeamua kwamba kinywa changu
hakitatenda dhambi.
Kuhusu matendo ya wanadamu:
kwa neno la midomo yako,
nimejiepusha
na njia za wenye jeuri.
Hatua zangu zimeshikamana na njia zako;
nyayo zangu hazikuteleza.
 
Ee Mungu, ninakuita, kwa kuwa utanijibu,
nitegee sikio lako na usikie ombi langu.
Uonyeshe ajabu ya upendo wako mkuu,
wewe uokoaye kwa mkono wako wa kuume
wale wanaokukimbilia kutokana na adui zao.
Nilinde kama mboni ya jicho lako,
unifiche chini ya kivuli cha mbawa zako
kutokana na waovu wanaonishambulia,
kutokana na adui wauaji wanaonizunguka.
 
10 Huifunga mioyo yao iliyo migumu,
vinywa vyao hunena kwa majivuno.
11 Wamenifuatia nyayo zangu, sasa wamenizingira,
wakiwa macho, waniangushe chini.
12 Wamefanana na simba mwenye njaa awindaye,
kama simba mkubwa anyemeleaye mafichoni.
 
13 Inuka, Ee Bwana, pambana nao, uwaangushe,
niokoe kutokana na waovu kwa upanga wako.
14 Ee Bwana, mkono wako uniokoe na watu wa jinsi hii,
kutokana na watu wa ulimwengu huu
ambao fungu lao liko katika maisha haya.
 
Na wapate adhabu ya kuwatosha.
Watoto wao na wapate zaidi ya hayo,
hukumu na iendelee kwa watoto wa watoto wao.
15 Na mimi katika haki nitauona uso wako,
niamkapo, nitaridhika kwa kuona sura yako.