Zaburi 29
Sauti Ya Bwana Wakati Wa Dhoruba
Zaburi ya Daudi.
Mpeni Bwana, enyi mashujaa,
mpeni Bwana utukufu na nguvu.
Mpeni Bwana utukufu unaostahili jina lake;
mwabuduni Bwana katika uzuri wa utakatifu wake.
Sauti ya Bwana iko juu ya maji;
Mungu wa utukufu hupiga radi,
Bwana hupiga radi juu ya maji makuu.
 
Sauti ya Bwana ina nguvu;
sauti ya Bwana ni tukufu.
Sauti ya Bwana huvunja mierezi;
Bwana huvunja vipande vipande
mierezi ya Lebanoni.
Hufanya Lebanoni irukaruke kama ndama,
Sirioni* urukaruke kama mwana nyati.
Sauti ya Bwana hupiga kwa miali
ya umeme wa radi.
Sauti ya Bwana hutikisa jangwa;
Bwana hutikisa Jangwa la Kadeshi.
Sauti ya Bwana huzalisha ayala,
na huuacha msitu wazi.
Hekaluni mwake wote wasema,
“Utukufu!”
 
10  Bwana huketi akiwa ametawazwa juu ya gharika;
Bwana ametawazwa kuwa Mfalme milele.
11  Bwana huwapa watu wake nguvu;
Bwana huwabariki watu wake kwa kuwapa amani.
* Zaburi 29:6 Yaani Mlima Hermoni.