Zaburi 40
Wimbo Wa Sifa
Kwa mwimbishaji. Zaburi ya Daudi.
Nilimngoja Bwana kwa saburi,
naye akaniinamia, akasikia kilio changu.
Akanipandisha kutoka shimo la uharibifu,
kutoka matope na utelezi;
akaiweka miguu yangu juu ya mwamba
na kunipa mahali imara pa kusimama.
Akaweka wimbo mpya kinywani mwangu,
wimbo wa sifa kwa Mungu wetu.
Wengi wataona na kuogopa
na kuweka tumaini lao kwa Bwana.
 
Heri mtu yule amfanyaye Bwana kuwa tumaini lake,
asiyewategemea wenye kiburi,
wale wenye kugeukia miungu ya uongo.
Ee Bwana Mungu wangu,
umefanya mambo mengi ya ajabu.
Mambo uliyopanga kwa ajili yetu
hakuna awezaye kukuhesabia;
kama ningesema na kuyaelezea,
yangekuwa mengi mno kuyaelezea.
 
Dhabihu na sadaka hukuvitaka,
lakini umefungua masikio yangu;*
sadaka za kuteketezwa na sadaka za dhambi
hukuzihitaji.
Ndipo niliposema, “Mimi hapa, nimekuja:
imeandikwa kunihusu katika kitabu.
Ee Mungu wangu,
natamani kuyafanya mapenzi yako;
sheria yako iko ndani ya moyo wangu.”
 
Nimehubiri haki katika kusanyiko kubwa,
sikufunga mdomo wangu,
Ee Bwana, kama ujuavyo.
10 Sikuficha haki yako moyoni mwangu;
ninasema juu ya uaminifu wako na wokovu wako.
Sikuficha upendo wako na kweli yako
mbele ya kusanyiko kubwa.
 
11 Ee Bwana, usizuilie huruma zako,
upendo wako na kweli yako daima vinilinde.
12 Kwa maana taabu zisizo na hesabu zimenizunguka,
dhambi zangu zimenikamata, hata nisiweze kuona.
Zimekuwa nyingi kuliko nywele za kichwa changu,
nao moyo unazimia ndani yangu.
 
13 Ee Bwana, uwe radhi kuniokoa;
Ee Bwana, njoo hima unisaidie.
14 Wote wanaotafuta kuuondoa uhai wangu,
waaibishwe na kufadhaishwa;
wote wanaotamani kuangamizwa kwangu,
warudishwe nyuma kwa aibu.
15 Wale waniambiao, “Aha! Aha!”
wafadhaishwe na iwe aibu yao.
16 Lakini wote wakutafutao
washangilie na kukufurahia,
wale wapendao wokovu wako siku zote waseme,
Bwana atukuzwe!”
 
17 Lakini bado mimi ni maskini na mhitaji;
Bwana na anifikirie.
Wewe ndiwe msaada wangu na Mwokozi wangu;
Ee Mungu wangu, usikawie.
* Zaburi 40:6 Au: bali mwili uliniandalia.