Zaburi 43
Maombi Ya Mtu Aliyeko Uhamishoni Yanaendelea
Ee Mungu unihukumu,
nitetee dhidi ya taifa lisilomcha Mungu,
niokoe na watu wadanganyifu na waovu.
Wewe ni Mungu ngome yangu.
Kwa nini umenikataa?
Kwa nini niendelee kuomboleza,
nikiwa nimeonewa na adui?
Tuma hima nuru yako na kweli yako
na viniongoze;
vinilete mpaka mlima wako mtakatifu,
mpaka mahali unapoishi.
Ndipo nitakwenda madhabahuni pa Mungu,
kwa Mungu, furaha yangu na shangwe yangu.
Nitakusifu kwa kinubi,
Ee Mungu, Mungu wangu.
 
Ee nafsi yangu, kwa nini unasononeka?
Kwa nini unafadhaika hivyo ndani yangu?
Weka tumaini lako kwa Mungu,
kwa sababu bado nitamsifu
Mwokozi wangu na Mungu wangu.