12
Kushukuru Na Kusifu
Katika siku ile utasema:
“Nitakusifu wewe, Ee Bwana.
Ingawa ulinikasirikia,
hasira yako imegeukia mbali
nawe umenifariji.
Hakika Mungu ni wokovu wangu;
nitamtumaini wala sitaogopa.
Bwana, Bwana, ni nguvu zangu na wimbo wangu;
amekuwa wokovu wangu.”
Kwa furaha mtachota maji
kutoka visima vya wokovu.
Katika siku hiyo mtasema:
“Mshukuruni Bwana, mliitie jina lake;
julisheni miongoni mwa mataifa yale aliyoyafanya,
tangazeni kuwa jina lake limetukuka.
Mwimbieni Bwana, kwa kuwa ametenda mambo makuu,
hili na lijulikane duniani kote.
Pazeni sauti mwimbe kwa furaha, watu wa Sayuni,
kwa maana mkuu ni yeye Aliye Mtakatifu wa Israeli miongoni mwenu.”