57
Ibada Ya Sanamu Ya Israeli Iliyo Batili
Mwenye haki hupotea,
wala hakuna hata mmoja awazaye hilo moyoni mwake;
watu wanaomcha Mungu huondolewa,
wala hakuna hata mmoja anayeelewa
kuwa wenye haki wameondolewa
ili wasipatikane na maovu.
Wale waendao kwa unyofu
huwa na amani;
hupata pumziko walalapo mautini.
 
“Lakini ninyi:
Njooni hapa, ninyi wana wa wachawi,
ninyi wazao wa wazinzi na makahaba!
Mnamdhihaki nani?
Ni nani mnayemcheka kwa dharau,
na kumtolea ndimi zenu?
Je, ninyi si watoto wa waasi,
uzao wa waongo?
Mnawaka tamaa katikati ya mialoni
na chini ya kila mti uliotanda matawi;
mnawatoa kafara watoto wenu kwenye mabonde
na chini ya majabali yenye mianya.
 
“Sanamu zilizo katikati ya mawe laini ya mabondeni ndizo fungu lenu;
hizo ndizo sehemu yenu.
Naam, kwa hizo mmemimina sadaka za vinywaji,
na kutoa sadaka za nafaka.
Katika haya yote,
niendelee kuona huruma?
Umeweka kitanda chako juu kwenye kilima kirefu kilichoinuka,
huko ulikwenda kutoa dhabihu zako.
Nyuma ya milango yako na miimo yako
umeweka alama zako za kipagani.
Kwa kuniacha mimi, ulifunua kitanda chako,
umepanda juu yake na kukipanua sana;
ulifanya patano na wale ambao unapenda vitanda vyao,
nawe uliangalia uchi wao.
Ulikwenda kwa Moleki* ukiwa na mafuta ya zeituni,
na ukaongeza manukato yako.
Ukawatuma wajumbe wako mbali sana,
ukashuka kwenye kaburi lenyewe!
10 Ulikuwa umechoshwa na njia zako zote,
lakini hukusema, ‘Hakuna tumaini.’
Ulipata uhuisho wa nguvu zako,
kwa sababu hiyo hukuzimia.
 
11 “Ni nani uliyemhofu hivyo na kumwogopa
hata ukawa mwongo kwangu,
wala hukunikumbuka
au kutafakari hili moyoni mwako?
Si ni kwa sababu nimekuwa kimya muda mrefu
hata huniogopi?
12 Nitaifunua haki yako na matendo yako,
nayo hayatakufaidi.
13 Utakapolia kwa kuhitaji msaada,
sanamu zako ulizojikusanyia na zikuokoe!
Upepo utazipeperusha zote,
pumzi peke yake itazipeperusha,
Lakini mtu atakayenifanya kimbilio lake,
atairithi nchi
na kuumiliki mlima wangu mtakatifu.”
Faraja Kwa Wenye Majuto
14 Tena itasemwa:
“Jengeni, jengeni, itengenezeni njia!
Ondoeni vikwazo katika njia ya watu wangu.”
15 Kwa maana hili ndilo asemalo Aliye juu, yeye aliyeinuliwa sana,
yeye aishiye milele, ambaye jina lake ni Mtakatifu:
“Ninaishi mimi mahali palipoinuka na patakatifu,
lakini pia pamoja na yeye aliye na roho iliyotubu
na mwenye roho ya unyenyekevu,
ili kuzihuisha roho za wanyenyekevu
na kuihuisha mioyo yao waliotubu.
16 Sitaendelea kulaumu milele,
wala sitakasirika siku zote,
kwa kuwa roho ya mwanadamu
ingezimia mbele zangu:
yaani pumzi ya mwanadamu niliyemuumba.
17 Nilighadhibika na tamaa yake ya dhambi;
nilimwadhibu, nikauficha uso wangu kwa hasira,
na bado aliendelea katika njia zake za tamaa.
18 Nimeziona njia zake, lakini nitamponya,
nitamwongoza na kumrudishia upya faraja,
19 nikiumba sifa midomoni ya waombolezaji
katika Israeli.
Amani, amani, kwa wale walio mbali
na kwa wale walio karibu,”
asema Bwana. “Nami nitawaponya.”
20 Bali waovu ni kama bahari ichafukayo,
ambayo haiwezi kutulia,
mawimbi yake hutupa takataka na matope.
21 Mungu wangu asema,
“Hakuna amani kwa waovu.”
* 57:9 Moleki alikuwa mungu aliyekuwa anaabudiwa na Waamoni; pia alijulikana kama Malkomu, Maloki au Kemoshi wa Moabu. 57:9 Kaburi hapa maana yake ni Kuzimu, kwa Kiebrania ni Sheol.