Zaburi 120
Kuomba Msaada
Wimbo wa kwenda juu.
Katika dhiki yangu namwita Bwana,
naye hunijibu.
Ee Bwana, uniokoe kutoka midomo ya uongo
na ndimi za udanganyifu.
 
Atakufanyia nini,
au akufanyie nini zaidi, ewe ulimi mdanganyifu?
Atakuadhibu kwa mishale mikali ya shujaa,
kwa makaa yanayowaka ya mti wa mretemu.
 
Ole wangu kwa kuwa naishi Mesheki,
kwamba naishi katikati ya hema za Kedari!
Nimeishi muda mrefu mno
miongoni mwa wale wanaochukia amani.
Mimi ni mtu wa amani;
lakini ninaposema, wao wanataka vita.