Zaburi 121
Bwana Mlinzi Wetu
Wimbo wa kwenda juu.
Nayainua macho yangu nitazame vilima,
msaada wangu utatoka wapi?
Msaada wangu hutoka kwa Bwana,
Muumba wa mbingu na dunia.
 
Hatauacha mguu wako uteleze,
yeye akulindaye hatasinzia,
hakika, yeye alindaye Israeli
hatasinzia wala hatalala usingizi.
Bwana anakulinda,
Bwana ni uvuli wako mkono wako wa kuume,
jua halitakudhuru mchana,
wala mwezi wakati wa usiku.
Bwana atakukinga na madhara yote,
atayalinda maisha yako,
Bwana atakulinda unapoingia na unapotoka,
tangu sasa na hata milele.