Zaburi 127
Bila Mungu, Kazi Ya Mwanadamu Haifai
Wimbo wa kwenda juu. Wa Solomoni.
Bwana asipoijenga nyumba,
wajengao hufanya kazi bure.
Bwana asipoulinda mji,
walinzi wakesha bure.
Mnajisumbua bure kuamka mapema
na kuchelewa kulala,
mkitaabikia chakula:
kwa maana yeye huwapa usingizi wapenzi wake.
 
Wana ni urithi utokao kwa Bwana,
watoto ni zawadi kutoka kwake.
Kama mishale mikononi mwa shujaa
ndivyo walivyo wana awazaao mtu katika ujana wake.
Heri mtu ambaye podo lake
limejazwa nao.
Hawataaibishwa wanaposhindana
na adui zao langoni.