Zaburi 13
Sala Ya Kuomba Msaada
Kwa mwimbishaji. Zaburi ya Daudi.
Mpaka lini, Ee Bwana? Je, utanisahau milele?
Utanificha uso wako mpaka lini?
Nitapambana na mawazo yangu mpaka lini,
na kila siku kuwa na majonzi moyoni mwangu?
Adui zangu watanishinda mpaka lini?
 
Nitazame, unijibu, Ee Bwana Mungu wangu.
Yatie nuru macho yangu,
ama sivyo nitalala usingizi wa mauti.
Adui yangu atasema, “Nimemshinda,”
nao adui zangu watashangilia nitakapoanguka.
 
Lakini ninategemea upendo wako usiokoma;
moyo wangu unashangilia katika wokovu wako.
Nitamwimbia Bwana,
kwa kuwa amekuwa mwema kwangu.