Zaburi 24
Mfalme Mkuu
Zaburi ya Daudi.
Dunia ni mali ya Bwana, na vyote vilivyomo ndani yake,
ulimwengu, na wote waishio ndani yake,
maana aliiwekea misingi yake baharini
na kuifanya imara juu ya maji.
 
Nani awezaye kuupanda mlima wa Bwana?
Ni nani awezaye kusimama patakatifu pake?
Ni yule mwenye mikono safi na moyo mweupe,
yule ambaye hakuinulia sanamu nafsi yake
au kuapa kwa kitu cha uongo.
Huyo atapokea baraka kutoka kwa Bwana,
na hukumu ya haki kutoka kwa Mungu Mwokozi wake.
Hiki ndicho kizazi cha wale wamtafutao,
wale wautafutao uso wako, Ee Mungu wa Yakobo.
 
Inueni vichwa vyenu, enyi malango,
inukeni enyi milango ya kale,
ili mfalme wa utukufu apate kuingia.
Ni nani huyu Mfalme wa utukufu?
Ni Bwana aliye na nguvu na uweza,
ni Bwana aliye hodari katika vita.
Inueni vichwa vyenu, enyi malango,
viinueni juu enyi milango ya kale,
ili Mfalme wa utukufu apate kuingia.
10 Ni nani yeye, huyu Mfalme wa utukufu?
Ni Bwana Mwenye Nguvu Zote;
yeye ndiye Mfalme wa utukufu.