Zaburi 60
Kuomba Kuokolewa
Kwa mwimbishaji. Mtindo wa “Shushani Eduthi.” Utenzi wa Daudi wa kufundisha. Wakati alipopigana na Waaramu kutoka Aramu-Naharaimu na Aramu-Soba, naye Yoabu akarudi nyuma na kuwaua Waedomu 12,000 katika Bonde la Chumvi.
Ee Mungu, umetukataa na kutokea ghafula juu yetu,
umekasirika: sasa turejeshe upya!
Umetetemesha nchi na kuipasua;
uiponye mavunjiko yake, kwa maana inatetemeka.
Umewaonyesha watu wako nyakati za kukata tamaa;
umetunywesha mvinyo unaotuyumbisha.
 
Kwa wale wanaokucha wewe,
umewainulia bendera,
ili iweze kutwekwa dhidi ya upinde.
 
Tuokoe na utusaidie kwa mkono wako wa kuume,
ili wale uwapendao wapate kuokolewa.
Mungu amenena kutoka patakatifu pake:
“Nitaigawa Shekemu kwa ushindi
na kulipima Bonde la Sukothi.
Gileadi ni yangu na Manase ni yangu;
Efraimu ni kofia yangu ya chuma,
nayo Yuda ni fimbo yangu ya utawala.
Moabu ni sinia langu la kunawia,
juu ya Edomu natupa kiatu changu;
nashangilia kwa kushindwa kwa Ufilisti.”
 
Ni nani atakayenipeleka hadi mji wenye ngome?
Ni nani atakayeniongoza hadi nifike Edomu?
10 Ee Mungu, si ni wewe uliyetukataa sisi,
na hutoki tena na majeshi yetu?
11 Tuletee msaada dhidi ya adui,
kwa maana msaada wa mwanadamu haufai kitu.
12 Kwa msaada wa Mungu tutapata ushindi,
naye atawaponda adui zetu.