Zaburi 61
Kuomba Ulinzi
Kwa mwimbishaji. Kwa ala za nyuzi za uimbaji. Zaburi ya Daudi.
Ee Mungu, sikia kilio changu,
usikilize maombi yangu.
 
Kutoka miisho ya dunia ninakuita,
ninaita huku moyo wangu unadhoofika;
uniongoze kwenye mwamba
ule ulio juu kuliko mimi.
Kwa kuwa umekuwa kimbilio langu,
ngome imara dhidi ya adui.
 
Natamani kukaa hemani mwako milele,
na kukimbilia chini ya uvuli wa mbawa zako.
Ee Mungu, kwa kuwa umesikia nadhiri zangu,
umenipa urithi wa wale wanaoliogopa jina lako.
 
Mwongezee mfalme siku za maisha yake,
miaka yake kwa vizazi vingi.
Yeye na atawazwe kwenye kiti cha enzi mbele za Mungu milele;
amuru upendo wako na uaminifu wako vimlinde.
 
Ndipo daima nitaliimbia sifa jina lako
na kuzitimiza nadhiri zangu siku baada ya siku.