Zaburi 78
Mungu Na Watu Wake
Utenzi wa Asafu.
Enyi watu wangu, sikieni mafundisho yangu,
sikilizeni maneno ya kinywa changu.
Nitafungua kinywa changu kwa mafumbo,
nitazungumza mambo yaliyofichika, mambo ya kale:
yale ambayo tuliyasikia na kuyajua,
yale ambayo baba zetu walituambia.
Hatutayaficha kwa watoto wao;
tutakiambia kizazi kijacho
matendo yastahiliyo sifa ya Bwana,
uweza wake, na maajabu aliyoyafanya.
Aliagiza amri kwa Yakobo
na akaweka sheria katika Israeli,
ambazo aliwaamuru baba zetu
wawafundishe watoto wao,
ili kizazi kijacho kizijue,
pamoja na watoto ambao watazaliwa,
nao pia wapate kuwaeleza watoto wao.
Ndipo wangeweka tumaini lao kwa Mungu,
nao wasingesahau matendo yake,
bali wangalizishika amri zake.
Ili wasifanane na baba zao,
waliokuwa kizazi cha ukaidi na uasi,
ambao roho zao hazikuwa na uaminifu kwake,
ambao roho zao hazikumwamini.
 
Watu wa Efraimu, ingawa walijifunga pinde,
walikimbia siku ya vita.
10 Hawakulishika agano la Mungu
na walikataa kuishi kwa sheria yake.
11 Walisahau aliyokuwa ameyatenda,
maajabu aliyokuwa amewaonyesha.
12 Alitenda miujiza machoni mwa baba zao,
huko Soani, katika nchi ya Misri.
13 Aliigawanya bahari akawapitisha,
alifanya maji yasimame imara kama ukuta.
14 Aliwaongoza kwa wingu mchana
na kwa nuru kutoka kwenye moto usiku kucha.
15 Alipasua miamba jangwani
na akawapa maji tele kama bahari,
16 alitoa vijito kutoka kwenye jabali lililochongoka,
akayafanya maji yatiririke kama mito.
 
17 Lakini waliendelea kutenda dhambi dhidi yake,
wakiasi jangwani dhidi ya Aliye Juu Sana.
18 Kwa makusudi walimjaribu Mungu,
wakidai vyakula walivyovitamani.
19 Walinena dhidi ya Mungu, wakisema,
“Je, Mungu aweza kuandaa meza jangwani?
20 Alipopiga mwamba, maji yalitoka kwa nguvu,
vijito vikatiririka maji mengi.
Lakini je, aweza kutupa chakula pia?
Je, anaweza kuwapa watu wake nyama?”
21  Bwana alipowasikia, alikasirika sana,
moto wake ukawa dhidi ya Yakobo,
na ghadhabu yake ikawaka dhidi ya Israeli,
22 kwa kuwa hawakumwamini Mungu,
wala kuutumainia ukombozi wake.
23 Hata hivyo alitoa amri kwa anga zilizo juu
na kufungua milango ya mbingu,
24 akawanyeshea mana ili watu wale;
aliwapa nafaka ya mbinguni.
25 Watu walikula mkate wa malaika,
akawatumia chakula chote ambacho wangeliweza kula.
26 Aliachia upepo wa mashariki kutoka kwenye mbingu
na kuuongoza upepo wa kusini kwa uwezo wake.
27 Aliwanyeshea nyama kama mavumbi,
ndege warukao kama mchanga wa pwani.
28 Aliwafanya washuke ndani ya kambi yao,
kuzunguka mahema yao yote.
29 Walikula na kusaza,
kwa maana alikuwa amewapa kile walichotamani.
30 Kabla hawajamaliza kula walichokitamani,
hata kilipokuwa kingali bado vinywani mwao,
31 hasira ya Mungu ikawaka juu yao,
akawaua wale waliokuwa na nguvu zaidi miongoni mwao,
akiwaangusha vijana wa Israeli.
 
32 Licha ya haya yote, waliendelea kutenda dhambi,
licha ya maajabu yake, hawakuamini.
33 Kwa hiyo akamaliza siku zao katika ubatili
na miaka yao katika vitisho.
34 Kila mara Mungu alipowaua baadhi yao,
waliosalia walimtafuta,
walimgeukia tena kwa shauku.
35 Walikumbuka kwamba Mungu alikuwa Mwamba wao,
kwamba Mungu Aliye Juu Sana alikuwa Mkombozi wao.
36 Lakini walimdanganya kwa vinywa vyao,
wakisema uongo kwa ndimi zao,
37 mioyo yao haikuwa thabiti kwake,
wala hawakuwa waaminifu katika agano lake.
38 Hata hivyo alikuwa na huruma,
alisamehe maovu yao
na hakuwaangamiza.
Mara kwa mara alizuia hasira yake,
wala hakuchochea ghadhabu yake yote.
39 Alikumbuka kwamba wao walikuwa nyama tu,
upepo upitao ambao haurudi.
 
40 Mara ngapi walimwasi jangwani
na kumhuzunisha nyikani!
41 Walimjaribu Mungu mara kwa mara,
wakamkasirisha yeye Aliye Mtakatifu wa Israeli.
42 Hawakukumbuka uwezo wake,
siku aliyowakomboa kutoka kwa mtesi,
43 siku aliyoonyesha ishara zake za ajabu huko Misri,
maajabu yake huko Soani.
44 Aligeuza mito yao kuwa damu,
hawakuweza kunywa maji kutoka vijito vyao.
45 Aliwapelekea makundi ya mainzi yakawala,
na vyura wakawaharibu.
46 Aliruhusu tunutu kuharibu mimea yao,
mazao yao kwa nzige.
47 Aliharibu mizabibu yao kwa mvua ya mawe
na mikuyu yao kwa mvua iliyochangamana na theluji.
48 Aliwaachia mifugo yao mvua ya mawe,
akayapiga makundi ya wanyama wao kwa radi.
49 Aliwafungulia hasira yake kali,
ghadhabu yake, hasira na uadui,
na kundi la malaika wa kuharibu.
50 Aliitengenezea njia hasira yake,
hakuwaepusha na kifo,
bali aliwaachia tauni.
51 Aliwapiga wazaliwa wote wa kwanza wa Misri,
matunda ya kwanza ya ujana katika mahema ya Hamu.
52 Lakini aliwatoa watu wake kama kundi,
akawaongoza kama kondoo kupitia jangwani.
53 Aliwaongoza salama, wala hawakuogopa,
bali bahari iliwameza adui zao.
54 Hivyo akawaleta hadi kwenye mpaka wa nchi yake takatifu,
hadi nchi ya vilima ambayo mkono wake wa kuume ulikuwa umeitwaa.
55 Aliyafukuza mataifa mbele yao,
na kuwagawia nchi zao kama urithi,
aliwakalisha makabila ya Israeli katika makao yao.
 
56 Lakini wao walimjaribu Mungu,
na kuasi dhidi ya Yeye Aliye Juu Sana,
wala hawakuzishika sheria zake.
57 Kama baba zao, hawakuwa thabiti wala waaminifu,
wakawa wasioweza kutegemewa
kama upinde wenye kasoro.
58 Wakamkasirisha Mungu kwa mahali pao pa juu pa kuabudia miungu,
wakachochea wivu wake kwa sanamu zao.
59 Wakati Mungu alipowasikia, alikasirika sana,
akamkataa Israeli kabisa.
60 Akaiacha hema ya Shilo,
hema aliyokuwa ameiweka katikati ya wanadamu.
61 Akalipeleka Sanduku la nguvu zake utumwani,
utukufu wake mikononi mwa adui.
62 Aliachia watu wake wauawe kwa upanga,
akaukasirikia sana urithi wake.
63 Moto uliwaangamiza vijana wao,
na wanawali wao hawakuimbiwa nyimbo za arusi,
64 makuhani wao waliuawa kwa upanga,
wala wajane wao hawakuweza kulia.
 
65 Ndipo Bwana alipoamka kama vile kuamka usingizini,
kama vile mtu aamkavyo kutoka kwenye bumbuazi la mvinyo.
66 Aliwapiga na kuwashinda adui zake,
akawatia katika aibu ya milele.
67 Ndipo alipozikataa hema za Yosefu,
hakulichagua kabila la Efraimu,
68 lakini alilichagua kabila la Yuda,
Mlima Sayuni, ambao aliupenda.
69 Alijenga patakatifu pake kama vilele,
kama dunia ambayo aliimarisha milele.
70 Akamchagua Daudi mtumishi wake
na kumtoa kwenye mazizi ya kondoo.
71 Kutoka kuchunga kondoo alimleta
kuwa mchungaji wa watu wake Yakobo,
wa Israeli urithi wake.
72 Naye Daudi aliwachunga kwa uadilifu wa moyo,
kwa mikono ya ustadi aliwaongoza.