KITABU CHA NNE
90
(Zaburi 90–106)
Umilele Wa Mungu Na Udhaifu Wa Mwanadamu
Maombi ya Mose, mtu wa Mungu.
Bwana, wewe umekuwa makao yetu
katika vizazi vyote.
Kabla ya kuzaliwa milima
au hujaumba dunia na ulimwengu,
wewe ni Mungu tangu milele hata milele.
 
Huwarudisha watu mavumbini,
ukisema, “Rudini mavumbini, enyi wanadamu.”
Kwa maana kwako miaka elfu
ni kama siku moja iliyokwisha pita,
au kama kesha la usiku.
Unawatowesha wanadamu katika usingizi wa kifo,
nao ni kama majani machanga ya asubuhi:
ingawa asubuhi yanachipua,
ifikapo jioni huwa yamenyauka na kukauka.
 
Tumeangamizwa kwa hasira yako
na tumetishwa kwa ghadhabu yako.
Umeyaweka maovu yetu mbele yako,
dhambi zetu za siri katika nuru ya uwepo wako.
Tumeishi siku zetu zote chini ya ghadhabu yako,
tunamaliza miaka yetu kwa kuomboleza.
10 Siku zetu za kuishi ni miaka sabini,
au miaka themanini ikiwa tuna nguvu,
lakini yote ni ya shida na taabu,
nazo zapita haraka, nasi twatoweka.
 
11 Ni nani ajuaye nguvu za hasira yako?
Kwa maana ghadhabu yako ni kubwa
kama hofu tunayopaswa kuwa nayo kwako.
12 Tufundishe kuzihesabu siku zetu vizuri,
ili tujipatie moyo wa hekima.
 
13 Ee Bwana, uwe na huruma! Utakawia hata lini?
Wahurumie watumishi wako.
14 Tushibishe asubuhi kwa upendo wako usiokoma,
ili tuweze kuimba kwa shangwe na kufurahi siku zetu zote.
15 Utufurahishe kulingana na siku ulizotuadhibu,
kulingana na miaka tuliyotaabika.
16 Matendo yako na yaonekane kwa watumishi wako,
utukufu wako kwa watoto wao.
 
17 Wema wa Bwana Mungu wetu uwe juu yetu;
uzithibitishe kazi za mikono yetu:
naam, uzithibitishe kazi za mikono yetu.