34
Yosia Afanya Matengenezo
(2 Wafalme 22:1-2)
Yosia alikuwa na miaka minane alipoanza kutawala, naye akatawala huko Yerusalemu miaka thelathini na mmoja. Akafanya yaliyo mema machoni pa Bwana na kuenenda katika njia za Daudi baba yake, hakugeuka upande wa kuume wala wa kushoto.
Katika mwaka wa nane wa utawala wake, alipokuwa angali bado mdogo, alianza kumtafuta Mungu wa Daudi baba yake. Katika mwaka wake wa kumi na mbili alianza kusafisha mahali pa juu pa kuabudia miungu pa Yuda na Yerusalemu, akiondoa nguzo za Ashera, sanamu za kuchonga na vinyago vya kusubu. Mbele ya macho yake, wakazibomoa madhabahu za Mabaali, wakazivunja madhabahu za kufukizia uvumba zilizokuwa zimesimama juu yake, wakazivunja nguzo za Ashera, sanamu na vinyago. Hivi alivivunja vipande vipande na kuvisambaza juu ya makaburi ya waliokuwa wamevitolea kafara. Akachoma mifupa ya makuhani wao juu ya madhabahu zao na kwa njia hiyo akaitakasa Yuda na Yerusalemu. Katika miji ya Manase, Efraimu na Simeoni, hadi Naftali na kwenye magofu yanayoizunguka, akavunja madhabahu na nguzo za Ashera na kuzipondaponda hizo sanamu hadi zikawa unga na kukata vipande vipande madhabahu zote za kufukizia uvumba katika Israeli yote. Kisha akarudi Yerusalemu.
Katika mwaka wa kumi na nane wa utawala wa Yosia, ili kutakasa nchi na Hekalu, akawatuma Shafani, mwana wa Azalia na Maaseya mtawala wa mji, pamoja na Yoa mwana wa Yoahazi, mwandishi ili kukarabati Hekalu la Bwana Mungu wake.
Wakamwendea Hilkia kuhani mkuu na kumpa fedha ambazo zilikuwa zimeletwa ndani ya Hekalu la Bwana ambazo Walawi waliokuwa mabawabu walikuwa wamezikusanya kutoka kwa watu wa Manase, Efraimu na mabaki wote wa Israeli kutoka kwa watu wote wa Yuda na Benyamini na wakazi wa Yerusalemu. 10 Kisha wakazikabidhi hizo fedha kwa watu waliowekwa ili kusimamia kazi ya Hekalu la Bwana. Hawa watu waliwalipa wafanyakazi waliokarabati na kutengeneza Hekalu lipate kurudi katika hali yake. 11 Wakawapa pia mafundi seremala na waashi fedha ili kununua mawe yaliyochongwa, mbao kwa ajili ya kufungia na boriti kwa ajili ya majengo ambayo wafalme wa Yuda walikuwa wameyaacha yakawa magofu.
12 Watu wakafanya kazi kwa uaminifu. Waliokuwa wamewekwa juu yao ili kuwaelekeza ni Yahathi na Obadia, Walawi wa uzao wa Merari, Zekaria na Meshulamu, waliotoka kwenye uzao wa Kohathi. Walawi wote waliokuwa na ufundi wa kupiga ala za uimbaji, 13 wakawa wasimamizi wa vibarua na kuwaongoza wale waliofanya kila aina ya kazi. Baadhi ya Walawi walikuwa waandishi, maafisa na mabawabu.
Kitabu Cha Sheria Chapatikana
(2 Wafalme 22:3-20)
14 Wakati walikuwa wakizitoa nje fedha zilizokuwa zimetolewa kwenye Hekalu la Bwana, kuhani Hilkia akakipata kile Kitabu cha Sheria ya Bwana kilichokua kimetolewa kwa mkono wa Mose. 15 Hilkia akamwambia Shafani mwandishi, “Nimekipata Kitabu cha Sheria ndani ya Hekalu la Bwana.” Akampa Shafani kile Kitabu.
16 Kisha Shafani akakipeleka kile Kitabu kwa mfalme na kumwambia, “Maafisa wako wanafanya kila kitu kama walivyokabidhiwa kufanya. 17 Wamelipa fedha zilizokuwa katika Hekalu la Bwana na wamewakabidhi wasimamizi na wafanyakazi.” 18 Kisha Shafani mwandishi akamwarifu mfalme kuwa, “Kuhani Hilkia amenipa Kitabu.” Naye Shafani akakisoma mbele ya mfalme.
19 Mfalme aliposikia yale maneno ya Sheria, akayararua mavazi yake. 20 Akatoa maagizo haya kwa Hilkia, Ahikamu mwana wa Shafani, Abdoni mwana wa Mika, Shafani mwandishi na Asaya mtumishi wa mfalme, 21 “Nendeni mkamuulize Bwana kwa ajili yangu na kwa ajili ya mabaki walioko Israeli na Yuda kuhusu yale yaliyoandikwa ndani ya kitabu hiki ambacho kimepatikana. Hasira ya Bwana ni kubwa mno ambayo imemwagwa juu yetu kwa sababu baba zetu hawakulishika neno la Bwana wala hawajatenda kulingana na yale yote yaliyoandikwa katika Kitabu hiki.”
22 Hilkia pamoja na wale wote mfalme aliokuwa amewatuma pamoja naye wakaenda kuzungumza na nabii mke aitwaye Hulda, aliyekuwa mke wa Shalumu mwana wa Tokhathi, mwana wa Hasra mtunzaji wa chumba cha mavazi. Hulda aliishi Yerusalemu, katika Mtaa wa Pili.
23 Akawaambia, “Hivi ndivyo asemavyo Bwana, Mungu wa Israeli: Mwambieni yule mtu aliyewatuma ninyi kwangu, 24 ‘Hivi ndivyo asemavyo Bwana: Nitaleta maafa juu ya mahali hapa na watu wake, laana zote zilizoandikwa ndani ya hicho kitabu ambazo zimesomwa mbele ya mfalme wa Yuda. 25 Kwa sababu wameniacha mimi na kufukiza uvumba kwa miungu mingine na kunighadhibisha kwa kazi yote ya mikono yao, hivyo hasira yangu itamwagwa juu ya mahali hapa, wala haitatulizwa.’ 26 Mwambieni mfalme wa Yuda, ambaye amewatuma kumuuliza Bwana, ‘Hivi ndivyo asemavyo Bwana, Mungu wa Israeli kuhusu maneno uliyoyasikia: 27 Kwa kuwa moyo wako ulikuwa msikivu na ulijinyenyekeza mbele za Mungu uliposikia kile nilichosema dhidi ya mahali hapa na watu wake na kwa sababu ulijinyenyekeza mbele zangu na uliyararua mavazi yako na kulia mbele zangu, nimekusikia, asema Bwana. 28 Basi nitakukusanya kwa baba zako, nawe utazikwa kwa amani. Macho yako hayataona maafa yote nitakayoleta juu ya mahali hapa na juu ya wote wanaoishi hapa.’ ”
Kwa hiyo wakampelekea mfalme jibu lake.
Yosia Afanya Agano La Kutii
(2 Wafalme 23:1-20)
29 Kisha mfalme akawaita pamoja wazee wote wa Yuda na Yerusalemu. 30 Akapanda kwenda hekaluni mwa Bwana pamoja na watu wa Yuda, watu wa Yerusalemu, makuhani na Walawi, watu wote, wakubwa kwa wadogo. Akasoma wakiwa wanasikia maneno yote ya Kitabu cha Agano, ambacho kilikuwa kimepatikana katika Hekalu la Bwana. 31 Mfalme akasimama karibu na nguzo yake na kufanya upya Agano mbele za Bwana ili kumfuata Bwana na kuzishika amri zake, maagizo na sheria kwa moyo wake wote na kwa roho yake yote na ili kuyatii maneno ya Agano yaliyoandikwa katika kitabu hiki.
32 Ndipo akamtaka kila mmoja katika Yerusalemu na Benyamini kuweka ahadi zao wenyewe kwa hilo Agano, watu wa Yerusalemu wakafanya hivyo kwa kufuata Agano la Bwana, Mungu wa baba zao.
33 Yosia akaondoa machukizo yote ya sanamu kutoka nchi yote iliyokuwa mali ya Waisraeli na akawataka wale wote waliokuwako katika Israeli wamtumikie Bwana Mungu wao. Kwa muda wote alioishi, hawakushindwa kumfuata Bwana, Mungu wa baba zao.