4
Vifaa Vya Hekalu
(1 Wafalme 7:23-51)
Mfalme Solomoni akatengeneza madhabahu ya shaba yenye urefu wa dhiraa ishirini,* upana wa dhiraa ishirini na kimo chake dhiraa kumi. Akatengeneza Bahari ya kusubu, yenye umbo la mviringo, ya dhiraa kumi kutoka ukingo hadi ukingo na kimo cha dhiraa tano. Kamba ya urefu wa dhiraa thelathini ingeweza kuizunguka. Chini ya huo ukingo, kulikuwa na mafahali kuizunguka, yaani mafahali kumi katika kila dhiraa moja.§ Hayo mafahali waliyasubu katika safu mbili yakiwa ya kitu kimoja na hiyo Bahari.
Bahari hiyo ilikaa juu ya mafahali kumi na wawili, mafahali watatu walielekeza nyuso zao kaskazini, watatu magharibi, watatu kusini na watatu mashariki. Bahari hiyo ilikaa juu ya hao mafahali, nazo sehemu zao za nyuma zilielekeana. Unene wake ulikuwa nyanda nne,* na ukingo wake ulifanana na ukingo wa kikombe, kama ua la yungiyungi iliyochanua. Iliweza kuchukua bathi 3,000.
Kisha akatengeneza masinia kumi kwa ajili ya kuoshea vifaa, naye akayaweka matano upande wa kusini na matano upande wa kaskazini. Ndani yake ndimo walioshea vifaa vya kutumika katika sadaka za kuteketezwa, lakini ile Bahari ilikuwa ni kwa ajili ya makuhani kunawia.
Akatengeneza vinara vya taa kumi vya dhahabu kama ilivyoainishwa kwao na kuviweka hekaluni, vinara vitano upande wa kusini na vitano upande wa kaskazini.
Akatengeneza meza kumi na kuziweka hekaluni, tano upande wa kusini na tano upande wa kaskazini. Pia akatengeneza mabakuli 100 ya dhahabu ya kunyunyizia.
Akatengeneza ukumbi wa makuhani na ukumbi mwingine mkubwa na milango yake, naye akaifunika hiyo milango kwa shaba. 10 Akaweka ile Bahari upande wa kusini, kwenye pembe ya kusini mashariki ya nyumba.
11 Pia akatengeneza masufuria, masepetu na mabakuli ya kunyunyizia.
Kwa hiyo Huramu akakamilisha kazi katika Hekalu la Mungu kama vile Mfalme Solomoni alikuwa amemwagiza, yaani:
 
12 zile nguzo mbili;
yale mataji mawili yaliyokuwa juu ya hizo nguzo,
zile nyavu mbili za kupamba hayo mataji mawili yenye umbo la bakuli yaliyowekwa juu ya zile nguzo;
13 yale makomamanga 400 kwa ajili ya hizo nyavu mbili (safu mbili za makomamanga kwa kila wavu yakipamba hayo mataji mawili yenye umbo la bakuli juu ya hizo nguzo);
14 vishikio pamoja na masinia yake;
15 hiyo Bahari na hao mafahali kumi na wawili chini yake;
16 pia hayo masufuria, masepetu, uma za nyama na vyombo vingine vyote vilivyohusiana.
 
Vitu vyote ambavyo Huramu-Abi alimtengenezea Mfalme Solomoni kwa ajili ya Hekalu la Bwana vilikuwa vya shaba iliyosuguliwa. 17 Mfalme aliagiza wavisubu vitu hivi kwenye kalibu za udongo wa mfinyanzi katika uwanda wa Yordani kati ya Sukothi na Sereda. 18 Vitu hivi vyote Mfalme Solomoni alivyotengeneza vilikuwa vingi sana hivi kwamba uzito wa shaba haungekadirika.
19 Solomoni pia akatengeneza samani zote zilizokuwa ndani ya Hekalu la Mungu:
 
madhabahu ya dhahabu;
meza za kuweka mikate ya Wonyesho;
20 vinara vya taa vya dhahabu safi pamoja na taa zake ili ziwake mbele ya sehemu takatifu ya ndani kama ilivyoelekezwa;
21 maua ya dhahabu yaliyofanyizwa, taa na makoleo (vilikuwa vya dhahabu bora kabisa);
22 mikasi ya dhahabu safi, mabakuli ya kunyunyizia, masinia na vyetezo; milango ya dhahabu ya Hekalu: yaani milango ya ndani ya Patakatifu pa Patakatifu, na milango ya ukumbi mkuu.
 
* 4:1 Dhiraa 20 ni sawa na mita 9. 4:1 Dhiraa 10 ni sawa na mita 4.5. 4:2 Dhiraa 30 ni sawa na mita 13.5. § 4:3 Dhiraa moja ni sawa na sentimita 45. * 4:5 Nyanda nne ni sawa na sentimita 7.5. 4:5 Bathi 3,000 ni sawa na lita 60,000. 4:17 Au Sarethani.