15
Watu fulani walishuka kutoka Uyahudi na kuwafundisha ndugu, wakisema, “msipotahiriwa kama desturi ya Musa, hamwezi kuokolewa.” Wakati Paulo na Barnaba walipokuwa na mapambano na mjadala pamoja nao, ndugu waliamua kwamba Paulo, Barnaba, na wengine kadhaa waende Yerusalem kwa mitume na wazee kwa ajili ya swali hili. Kwa hiyo, kwa kutumwa kwao na kanisa, walipitia Foinike na Samaria wakitangaza kugeuzwa nia kwa wamataifa. Walileta furaha kuu kwa ndugu wote, Walipokuja Yerusalem, walikaribishwa na Kanisa na mitume na wazee, na waliwasilisha taarifa ya mambo yote ambayo Mungu amefanya pamoja nao. Lakini watu fulani walioamini, waliokuwa katika kundi la Mafarisayo, walisimama nakusema, “ni muhimu kuwatahiri na kuwaamuru waishike sheria ya Musa.” Hivyo mitume na wazee walisimama pamoja kulifikiria hili swala. Baada ya majadiliano marefu, Petro alisimama na kusema kwao, “Ndugu mwatambua kwamba kitambo kizuri kilichopita Mungu alifanya chaguo kati yenu, kwamba kwa mdomo wangu Mataifa wasikie neno la injili, na kuamini. Mungu, anayefahamu mioyo, anashuhudia kwao, anawapa Roho mtakatifu, kama alivyofanya kwetu; na hakutengeneza utofauti kati yetu na wao, akiifanya mioyo yao safi kwa imani. 10 Kwa hiyo, kwa nini mnamjaribu Mungu kwamba muweke nira juu ya shingo za wanafunzi ambayo hata baba zetu wala sisi hatukuweza kustahimili? 11 Lakini twaamini kwamba tutaokolewa kwa neema ya Bwana Yesu, kama walivyokuwa.” 12 Kusanyiko lote lilinyamaza walipokua wakimsikiliza Barnaba na Paulo walipokuwa wakitoa taarifa ya ishara na maajabu ambayo Mungu alifanya pamoja nao kati ya watu wa mataifa. 13 Walipoacha kuongea, Yakobo alijibu akisema, “Ndugu nisikilizeni. 14 Simoni ameelezea jinsi kwanza Mungu kwa neema aliwasaidia Mataifa ili kwamba ajipatie kutoka kwao watu kwa ajili ya jina lake. 15 Maneno ya manabii yanakubaliana na hili kama lilivyoandikwa. 16 'Baada ya mambo haya nitarudi na kuijenga tena hema ya Daudi, iliyoanguka chini; nitainua na kuhuisha uhararibifu wake, 17 ili kwamba watu waliobaki wamtafute Bwana, pamoja na watu wa Mataifa walioitwa kwa jina langu.' 18 Hivi ndivyo asemavyo Bwana aliyefanya mambo haya yajulikanayo tangu enzi za zamani. 19 Hivyo basi, ushauri wangu ni, kwamba tusiwapatie shida watu wa Mataifa wamgeukiao Mungu; 20 lakini tuandike kwao kwamba wajiepushe mbali na uharibifu wa sanamu, tamaa za uasherati, na vilivyonyongwa, na damu. 21 Kutoka vizazi vya wazee kuna watu katika kila mji wahubirio na kumsoma Musa katika masinagogi kila Sabato.” 22 Kwa hiyo ikaonekana kuwa imewapendeza mitume na wazee, pamoja na kanisa lote, kumchagua Yuda aliyeitwa Barsaba, na Silas, waliokuwa viongozi wa kanisa, na kuwatuma Antiokia pamoja na Paulo na Barnaba. 23 Waliandika hivi, “Mitume, wazee na ndugu, kwa ndugu wa Mataifa walioko Antiokia, Shamu na Kilikia, salamu. 24 Tulisika kwamba watu fulani ambao hatukuwapatia amri hiyo, walitoka kwetu na wamewataabisha kwa mafundisho yaletayo shida nafsini mwenu. 25 Kwa hiyo imeonekana vyema kwetu sote kuchagua watu na kuwatuma kwenu pamoja na wapendwa wetu Barnaba na Paulo, 26 watu walio hatarisha maisha yao kwa ajili ya jina la Bwana Yesu Kristo. 27 Kwa hiyo tumemtuma Yuda na Sila, watawaambia mambo yayo hayo. 28 Kwa kuwa ilionekana vyema kwa Roho Mtakatifu na kwetu, kutoweka juu yenu mzigo mkubwa kuliko mambo haya yaliyo ya lazima: 29 kwamba mgeuke kutoka kwenye vitu vitolewavyo kwa sanamu, damu, vitu vya kunyongwa, na uasherati. Kama mtajiweka mbali na hivi, itakuwa vyema kwenu. Kwa herini.” 30 Hivyo basi, walivyotawanyishwa, waliteremkia Antiokia; baada ya kukusanya kusanyiko pamoja, waliwasilisha barua. 31 Walipokua wameisoma, walifurahi kwa sababu ya kutiwa moyo. 32 Yuda na Sila, na manabii, waliwatia moyo ndugu kwa maneno mengi na kuwatia nguvu. 33 Baada ya kukaa muda fulani huko, walitawanyishwa kwa amani kutoka kwa ndugu kwa wale waliowatuma. 34 [ Lakini ilionekana vyema Sila kubaki huko ] 35 Lakini Paulo na wengine walikaa Antiokia pamoja na wengine wengi, ambapo walifundisha na kuhubiri neno la Bwana. 36 Baada ya siku kadhaa Paulo alisema kwa Barnaba, “Na turudi sasa na kuwatembelea ndugu katika kila mji tulipohubiri neno la Bwana, na kuwaona walivyo. 37 Barnaba alihitaji pia kumchukua pamoja nao Yohana aliyeitwa Marko. 38 Lakini Paulo alifikiria haikuwa vizuri kumchukua Marko, aliyewaacha huko Pamfilia na hakuendelea nao katika kazi. 39 Kisha hapo kukatokea mabishano makubwa kwa hiyo walitengana, na Barnaba alimchukua Marko na kusafiri kwa meli mpaka Kipro, 40 Lakini Paulo alimchagua Sila na kuondoka, baada ya kukabidhiwa na ndugu katika neema ya Bwana. 41 Na alienda kupitia Shamu na Kilikia, akiimarisha makanisa.