Warumi
1
Paulo, mtumishi wa Yesu Kristo, aliyeitwa kuwa mtume, na kutengwa kwa ajili ya Injili ya Mungu. Hii ndio ile Injili aliyoiahidi zamani kupitia manabii wake katika maandiko matakatifu. Ni kuhusu Mwana wake, aliyezaliwa kutoka ukoo wa Daudi kwa jinsi ya mwili. Yeye alitangazwa kwa Mwana wa Mungu kwa nguvu ya Roho ya utakatifu kwa ufufuo wa wafu, Yesu Kristo Bwana wetu. Kupitia yeye tumepokea neema na utume kwa utii wa imani kati ya mataifa yote, kwa ajili ya jina lake. Kati ya mataifa haya, ninyi pia mmeitwa kuwa wa Yesu Kristo. Barua hii ni kwa wote walioko Rumi, wapendwao na Mungu, walioitwa kuwa watu watakatifu. Neema na iwe kwenu, na amani kutoka kwa Mungu Baba yetu na Bwana Yesu Kristo. Kwanza, namshukuru Mungu wangu katika Yesu Kristo kwa ajili yenu nyote, kwa sababu imani yenu inahubiriwa katika dunia nzima. Kwa maana Mungu ni shahidi wangu, ambaye ninamtumikia kwa roho yangu katika injili ya Mwana wake, jinsi ninavyodumu katika kuwataja. 10 Daima naomba katika sala zangu kwamba kwa njia yoyote nipate mwishowe kuwa na mafanikio sasa kwa mapenzi ya Mungu katika kuja kwenu. 11 Maana natamani kuwaona, ili nipate kuwapa ninyi baadhi ya karama za rohoni, nipate kuwaimarisha. 12 Yaani, natazamia kutiwa moyo pamoja nanyi, kwa njia ya imani ya kila mmoja wetu, yenu na yangu. 13 Sasa ndugu, sitaki mkose kufahamu kwamba, mara nyingi nimekusudia kuja kwenu, lakini nimezuiliwa mpaka sasa. Nilitaka hivi ili kuwa na matunda kwenu kama ilivyo pia miongoni mwa watu wa mataifa. 14 Nadaiwa na Wayunani na wageni pia, werevu na wajinga. 15 Kwa hiyo, kwa upande wangu, mimi niko tayari kutangaza injili kwenu pia ninyi mlio huko Roma. 16 Kwa maana siionei haya injili, kwa kuwa ni uweza wa Mungu uletao wokovu kwa kila aaminiye, kwa Myahudi kwanza na kwa Myunani pia. 17 Kwa maana haki ya Mungu imedhihirishwa kutoka imani hata imani, kama ilivyo andikwa, “Mwenye haki ataishi kwa imani.” 18 Maana ghadhabu ya Mungu imedhihirishwa kutoka mbinguni dhidi ya uasi na uovu wote wa watu, ambao kwa njia ya udhalimu huificha kweli. 19 Hii ni kwa sababu, yote yanayoweza kujulikana juu ya Mungu ni wazi kwao. Maana Mungu amewafahamisha. 20 Maana mambo yake yasioonekana vizuri yamekuwa wazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu. Yanaeleweka kupitia vitu vilivyoumbwa. Mambo haya ni uwezo wake wa milele na asili ya uungu. Matokeo yake, watu hawa hawana udhuru. 21 Hii ni kwa sababu, ingawa walijua kuhusu Mungu, hawakumtukuza yeye kama Mungu, wala hawakumpa shukrani. Badala yake, wamekuwa wapumbavu katika mawazo yao, na mioyo yao yenye ujinga ilitiwa giza. 22 Walijiita kuwa ni werevu, lakini wakawa wajinga. 23 Waliubadili utukufu wa Mungu asie na uharibifu kwa mfano wa sura ya binadamu aliye na uharibifu, na ya ndege, ya wanyama wenye miguu minne, na ya viumbe vitambaavyo. 24 Kwa hiyo Mungu aliwaacha wafuate tamaa za mioyo yao kwa uchafu, kwa miili yao kufedheheshwa baina yao. 25 Ni wao walioibadili kweli ya Mungu kuwa uongo, na ambao waliabudu na kutumikia viumbe badala ya Muumbaji, ambaye anasifiwa milele. Amina. 26 Kwa sababu hii, Mungu aliwaacha wafuate tamaa zao za aibu, kwa kuwa wanawake wao walibadilisha matumizi yao ya asili kwa kile kilicho kinyume na asili. 27 Hali kadhalika, wanaume pia wakaacha matumizi yao ya asili kwa wanawake na kuwakwa na tamaa dhidi yao wenyewe. Hawa walikuwa wanaume ambao walifanya na wanaume wenzao yasiyo wapasa, na ambao walipokea adhabu iliyostahili upotovu wao. 28 Kwa sababu walikataa kuwa na Mungu katika fahamu zao, aliwaacha wafuate akili zao zisizofaa, wafanye mambo yale yasiyofaa. 29 Wamejawa na udhalimu wote, uovu, tamaa na ubaya. Wamejawa na wivu, uuaji, ugomvi, udanganyifu, na nia mbaya. 30 Wao pia ni wasengenyaji, wasingiziaji, na wenye kumchukia Mungu. Wenye vurugu, kiburi, na majivuno. Wao ni watunga mabaya, na wasiotii wazazi wao. 31 Wao hawana ufahamu; wasioaminika, hawana mapenzi ya asili, na wasio na huruma. 32 Wanaelewa kanuni za Mungu, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo wanastahili kifo. Lakini si tu wanafanya mambo hayo, wao pia wanakubaliana na wale wanaofanya mambo hayo.