Zaburi 113
Kumsifu Bwana Kwa Wema Wake
Msifuni Bwana.
 
Enyi watumishi wa Bwana msifuni,
lisifuni jina la Bwana.
Jina la Bwana na lisifiwe,
sasa na hata milele.
Kuanzia mawio ya jua hadi machweo yake,
jina la Bwana linapaswa kusifiwa.
 
Bwana ametukuka juu ya mataifa yote,
utukufu wake juu ya mbingu.
Ni nani aliye kama Bwana Mungu wetu,
Yeye ambaye ameketi juu kwenye kiti cha enzi,
ambaye huinama atazame chini
aone mbingu na nchi?
 
Huwainua maskini kutoka mavumbini,
na kuwanyanyua wahitaji kutoka kwenye jalala,
huwaketisha pamoja na wakuu,
pamoja na wakuu wa watu wake.
Humjalia mwanamke tasa kutulia nyumbani mwake,
akiwa mama watoto mwenye furaha.
 
Msifuni Bwana.