Zaburi 148
Mwito Kwa Ulimwengu Kumsifu Mungu
Msifuni Bwana.
 
Msifuni Bwana kutoka mbinguni,
msifuni juu vileleni.
Msifuni, enyi malaika wake wote,
msifuni yeye, enyi jeshi lake lote la mbinguni.
Msifuni yeye, enyi jua na mwezi,
msifuni yeye, enyi nyota zote zingʼaazo.
Msifuni yeye, enyi mbingu zilizo juu sana,
na ninyi maji juu ya anga.
Vilisifu jina la Bwana
kwa maana aliamuru navyo vikaumbwa.
Aliviweka mahali pake milele na milele,
alitoa amri ambayo haibadiliki milele.
 
Mtukuzeni Bwana kutoka duniani,
ninyi viumbe vikubwa vya baharini na vilindi vyote vya bahari,
umeme wa radi na mvua ya mawe, theluji na mawingu,
pepo za dhoruba zinazofanya amri zake,
ninyi milima na vilima vyote,
miti ya matunda na mierezi yote,
10 wanyama wa mwituni na mifugo yote,
viumbe vidogo na ndege warukao,
11 wafalme wa dunia na mataifa yote,
ninyi wakuu na watawala wote wa dunia,
12 wanaume vijana na wanawali,
wazee na watoto.
 
13 Wote na walisifu jina la Bwana,
kwa maana jina lake pekee limetukuka,
utukufu wake uko juu ya nchi na mbingu.
14 Amewainulia watu wake pembe,*
sifa ya watakatifu wake wote,
ya Israeli, watu walio karibu na moyo wake.
 
Msifuni Bwana.
* Zaburi 148:14 Pembe hapa inawakilisha mwenye nguvu, yaani mfalme.