Zaburi 7
Sala Ya Mtu Anayedhulumiwa
Ombolezo la Daudi kwa Bwana kwa sababu ya Kushi, Mbenyamini.
Ee Bwana, Mungu wangu, ninakukimbilia wewe,
uniokoe na kunikomboa na wote wanaonifuatia,
la sivyo watanirarua kama simba
na kunichana vipande vipande, asiwepo wa kuniokoa.
 
Ee Bwana, Mungu wangu, kama nimetenda haya
na kuna hatia mikononi mwangu,
au ikiwa nimemtenda uovu aliye na amani nami,
au nimemnyangʼanya adui yangu pasipo sababu,
basi adui anifuatie na kunipata,
auponde uhai wangu ardhini
na kunilaza mavumbini.
 
Amka kwa hasira yako, Ee Bwana,
inuka dhidi ya ghadhabu ya adui zangu.
Amka, Mungu wangu, uamue haki.
Kusanyiko la watu na likuzunguke.
Watawale kutoka juu.
Bwana na awahukumu kabila za watu.
Nihukumu Ee Bwana,
kwa kadiri ya haki yangu,
kwa kadiri ya uadilifu wangu,
Ewe Uliye Juu Sana.
Ee Mungu mwenye haki,
uchunguzaye mawazo na mioyo,
komesha ghasia za waovu
na ufanye wenye haki waishi kwa amani.
 
10 Ngao langu ni Mungu Aliye Juu Sana,
awaokoaye wanyofu wa moyo.
11 Mungu ni mwamuzi mwenye haki,
Mungu aghadhibikaye kila siku.
12 Kama hakutuhurumia,
atanoa upanga wake,
ataupinda na kuufunga uzi upinde wake.
13 Ameandaa silaha zake kali,
ameweka tayari mishale yake ya moto.
 
14 Yeye aliye na mimba ya uovu
na achukuaye mimba ya ghasia huzaa uongo.
15 Yeye achimbaye shimo na kulifukua
hutumbukia katika shimo alilochimba mwenyewe.
16 Ghasia azianzishazo humrudia mwenyewe,
ukatili wake humrudia kichwani.
 
17 Nitamshukuru Bwana kwa ajili ya haki yake,
na nitaliimbia sifa jina la Bwana Aliye Juu Sana.