Zaburi 86
Kuomba Msaada
Maombi ya Daudi.
Ee Bwana, sikia na unijibu,
kwa maana mimi ni maskini na mhitaji.
Linda maisha yangu, kwa maana nimejiweka kwako,
wewe ni Mungu wangu,
mwokoe mtumishi wako anayekutumaini.
Ee Bwana, nihurumie mimi,
kwa maana ninakuita mchana kutwa.
Mpe mtumishi wako furaha,
kwa kuwa kwako wewe, Ee Bwana,
ninainua nafsi yangu.
 
Ee Bwana, wewe ni mwema na mwenye kusamehe,
umejaa upendo kwa wote wakuitao.
Ee Bwana, sikia maombi yangu,
sikiliza kilio changu unihurumie.
Katika siku ya shida yangu nitakuita,
kwa maana wewe utanijibu.
 
Ee Bwana, katikati ya miungu hakuna kama wewe,
hakuna matendo ya kulinganishwa na yako.
Ee Bwana, mataifa yote uliyoyafanya
yatakuja na kuabudu mbele zako;
wataliletea utukufu jina lako.
10 Kwa maana wewe ni mkuu, na unafanya mambo ya ajabu;
wewe peke yako ndiwe Mungu.
 
11 Ee Bwana, nifundishe njia yako,
nami nitakwenda katika kweli yako;
nipe moyo usiositasita,
ili niweze kulicha jina lako.
12 Ee Bwana wangu, nitakusifu kwa moyo wote;
nitaliadhimisha jina lako milele.
13 Kwa maana upendo wako ni mkuu kwangu;
umeniokoa kutoka kwenye vilindi vya kaburi.*
 
14 Ee Mungu, wenye majivuno wananishambulia;
kundi la watu wakatili linatafuta uhai wangu:
watu wasiokuheshimu wewe.
15 Lakini wewe, Ee Bwana, ni Mungu wa huruma na neema,
si mwepesi wa hasira, bali ni mwingi wa upendo na uaminifu.
16 Nigeukie na unihurumie;
mpe mtumishi wako nguvu zako,
mwokoe mwana wa mtumishi wako wa kike.
17 Nipe ishara ya wema wako,
ili adui zangu waione nao waaibishwe,
kwa kuwa wewe, Ee Bwana,
umenisaidia na kunifariji.
* Zaburi 86:13 Yaani Kuzimu. Zaburi 86:16 Au: mwokoe mwanao mwaminifu.