68
Kwa kiongozi wa muziki; Zaburi ya Daudi, wimbo. Mungu ainuke, maadui zake watawanyike; pia wale wamchukiao wakimbie mbele zake. Kama moshi uondoshwavyo, hivyo uwaondoshe wao; kama nta iyeyukavo mbele ya moto, hivyo waovu waangamizwe uweponi mwa Mungu. Bali wenye haki wafurahi; washangilie mbele za Mungu; washangilie na kufurahi. Mwimbieni Mungu! Lisifuni jina lake! Msifuni yule aendeshaye farasi kwenye tambarare ya bonde la Mto Yordani! Yahwe ni jina lake! Shangilieni mbele zake! Baba wa yatima, na mwamuzi wa wajane, ni Mungu anayeishi mahali patakatifu. Mungu huwaweka wakiwa katika familia; yeye huwafungua wafungwa kwa kuimba bali waasi huishi katika ardhi kavu. Mungu, wewe ulipoenda mbele ya watu wako, ulipotembea kupitia jangwani, Selah nchi ilitetemeka; mbingu pia zilidondosha mvua katika uwepo wa Mungu, uweponi mwa Mungu wakati alipokuja Sinai, uweponi mwa Mungu, Mungu wa Israeli. Wewe, Mungu, ulituma mvua nyingi; uliuimarisha urithi wako wakati ulipokuwa umechoka. 10 Watu wako waliishi humo; Wewe, Mungu, uliutoa kwa wema wako kwa maskini. 11 Bwana alitoa amri, na wale walio zitangaza walikuwa ni jeshi kuu. 12 Wafalme wa majeshi wanakimbia, wanakimbia, na wanawake wakisubiri nyumbani kuvigawana wao na familia zao vilivyotekwa nyara. 13 Njiwa walio vikwa fedha wakiwa na mabawa ya njano ya dhahabu. Wakati baadhi ya watu wakikaa kati ya mifugo ya kondoo, kwa nini umefanya haya? 14 Mwenyezi Mungu aliwatawanya Wafalme huko, ilikuwa kama vile wakati wa theluji juu ya Mlima Salmoni. 15 Mlima mkubwa ni milima wa mji wa Bashani; mlima mrefu ni mlima wa mji wa Bashani. 16 Ewe mlima mrefu wa nchi, kwa nini unatazama kwa jicho la husuda, kwenye mlima ambao Mungu ameutaka kwa ajili ya mahali ambapo yeye ataishi? Hakika, Yahwe ataishi humo milele. 17 Magari ya Mungu ni ishirini elfu, maelfu juu ya maelfu; Bwana yu kati yao katika mahari patakatifu, kama katika Sinai. 18 Wewe umepaa juu; uliwaongoza mateka; umepokea zawadi kutoka kati ya watu, hata kutoka kwa wale waliopigana dhidi yako, ili kwamba wewe, Yahwe Mungu, uweze kuishi huko. 19 Abarikiwe Bwana, atubebeaye mizigo yetu, Mungu ambaye ni wokovu wetu. Selah 20 Mungu wetu ni Mungu aokoaye; Yahwe Bwana ni yule awezaye kutuokoa sisi dhidi ya kifo. 21 Lakini Bwana atapiga vichwa vya adui zake, mpaka kwenye ngozi ya kichwa yenye nywele ya wale watembeao katika makosa dhidi yake. 22 Bwana alisema, “Nitawarudisha adui zangu kutoka Bashani; nitawarudisha kutoka katika kina cha bahari 23 ili kwamba upate kuwaangamiza adui zako, ukichovya mguu wako katika damu, na ili kwamba ndimi za mbwa wako zipate mlo wao kutoka kwa adui zenu.” 24 Mungu, wameona maandamano yako, maandamano ya Mungu wangu, Mfalme wangu, kwenye mahali patakatifu. 25 Waimbaji walitangulia, walifuatiwa na wapiga muziki, na katikati walikuwa wanawali wakicheza ngoma. 26 Mtukuzeni Mungu katika kusanyiko; msifuni Yahwe, ninyi ukoo wa kweli wa Israeli. 27 Kuna Benjamini kwanza, kabila dogo, kisha viongozi wa Yuda na watu wao, viongozi wa Zabuloni na viongozi wa Naftali. 28 Mungu wenu, Israeli, ameamuru nguvu zenu; uzifunue kwetu nguvu zako, Mungu, kama ulivyo zifunua wakati uliopita. 29 Uzifunue nguvu zako kwetu toka katika hekalu la Yerusalemu, ambako wafalme huleta zawadi kwako. 30 Pigeni kelele katika vita dhidi ya wanyama wa porini katika mianzi, dhidi ya watu, lile kundi la mafahari na ndama. Wafedhehesheni na kuwalazimisha wawaletee zawadi; watawanyeni watu wapendao kupigana vita. 31 Wakuu watatoka katika Misri; Ethiopia itafanya haraka kuufikisha mkono wake kwa Mungu. 32 Mwimbieni Mungu, enyi falme za nchi; Selah mwimbieni sifa Yahwe. 33 Kwake yeye apitaye juu ya mbingu za mbingu, zilizokuwepo tangu zama za kale; tazama, yeye hupiga kelele kwa nguvu 34 Tangazeni kuwa Mungu ni mwenye nguvu; enzi yake iko juu ya Israeli, na nguvu zake ziko angani. 35 Mungu, mahali pako patakatifu panatisha; Mungu wa Israeli, yeye huwapa watu wake nguvu na uweza. Atukuzwe Mungu.